Header Ads

Picha na Hotuba Rasmi:Maofisi Utamaduni Waaswa Kukusanya Takwimu za Ubunifu wa Sanaa na Utamaduni Nchini

Picha na Hotuba Rasmi:Maofisi Utamaduni Waaswa Kukusanya Takwimu za Ubunifu wa Sanaa na Utamaduni Nchini


Mkurugenzi wa Utamaduni toka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Prof. Hermas Mwansoko akisisitiza jambo wakati wa ufunguzi wa semina ya siku tatu juu ukusanyaji wa takwimu za kazi za ubunifu wa sanaa na utamaduni mapema hii leo jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu  toka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Barnabas Ndunguru akifungua semina ya siku tatu  kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bibi Sihaba Nkinga juu ya umuhimu wa ukusanyaji wa takwimu za kazi za ubunifu wa sanaa na utamaduni mapema hii leo jijini Dar es Salaam.

Mtakwimu Mwandamizi toka Jumuiya ya Afrika Mashariki Bw. Robert Maate  akielezea umuhimu wa ukusnyaji takwimu za kazi za ubunifu wa sanaa na utamaduni wakati wa semina ya siku tatu mapema hii leo jijini Dar es Salaam.

Afisa Mkuu wa Utamaduni na Michezo  toka Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki Bw. Bakaye Lubega akifafanua jambo wakati wa semina ya siku tatu juu ya ukusanyaji wa takwimu za kazi za ubunifu wa sanaa na utamaduni iliyofanyika mapema hii leo jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya washiriki wa semina ya siku tatu  juu ya ukusanyaji wa takwimu za kazi za ubunifu wa sanaa na utamaduni wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa inawasilishwa na Mtakwimu Mwandamizi toka Jumuiya ya Afrika Mashariki Bw. Robert Maate (hayupo pichani) mapema hii leo jijini Dar es Salaam.Picha na Eliphace Marwa
-- 
JAMHURI YA MUUGANO WA TANZANIA
WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO
HOTUBA YA KATIBU MKUU WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO BIBI SIHABA NKINGA  , WAKATI WA UFUNGUZI WA WARSHA YA MAFUNZO YA UKUSANYAJI TAKWIMU ZA UBUNIFU WA SANAA NA UTAMADUNI NCHINI TANZANIA, JB BELMONT HOTEL,DAR ES SALAAM, TAREHE 9 JUNI, 2014
--
Ndugu Wanawarsha,
Awali ya yote napenda kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa kunipatia fursa hii ya kuwa Mgeni Rasmi katika mafunzo haya mafupi ya ukusanyaji wa takwimu za ubunifu wa sanaa na utamaduni nchini Tanzania “Mapping Study of Culture and Creative Industries in EAC” – Tanzania Chapter.
Ndugu Wanawarsha,
Napenda kuwapongeza wale wote waliohusika kwa maandalizi mazuri ya kazi hii, hasa Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki, wakishirikiana na wataalamu wa Wizara yangu.
Kutokana na umuhimu wa mafunzo na kazi itakayofanywa baada ya mafunzo, sina budi kuwapongeza pia watumishi wa Serikali mliobahatika kuchaguliwa kushiriki kwenye programu hii.  Fursa hii hamkupewa kama zawadi, bali imetokana na kutambua juhudi na kujituma kwenu kazini na raghba yenu ya kumakinikia masuala yanayohusu utamaduni.  Hivyo, nakuombeni mwendelee na umakinifu wenu wakati wote wa mafunzo na zoezi la ukusanyaji takwimu.
Tena nyie mna bahati kubwa, kwani mnayo fursa ya kutumia uzoefu walioupata wanajumuiya wenzetu kutoka Kenya, Uganda na Burundi, ambako mafunzo na utafiti huu vimeshafanywa.  Hivyo, ni matarajio yangu kwamba nyie mtaitekeleza programu hii ya mafunzo na ukusanyaji takwimu za ubunifu wa kazi za sanaa na utamaduni kwa ufanisi mkubwa.
Ndugu Wanawarsha,
Kwa muda mrefu kumekuwepo nchini mwetu na dhana kuwa pamoja na amali nyingi za sanaa na utamaduni tulizonazo, bado hatujawa na usahihi wa sindano wa idadi kamili ya amali hizo.  Aidha, hatuna taarifa za uhakika wa jinsi amali hizo zinavyochangia kimapato sio tu kwa wasanii wenyewe, bali pia katika pato la Taifa.  Lengo la programu hii iliyoasisiwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki ni kupata majawabu kuntu kwa maeneo yote haya ya uelewa wenye ukakasi kwa nchi zote wanachama wa Jumuiya.
Kwa maneno mengine, zoezi hili la ukusanyaji wa takwimu za ubunifu wa sanaa na utamaduni litasaidi kwa kiasi kikubwa kujua hali halisi ya sasa ya amali za utamaduni na mustakabali wake wa baadaye kwenye uchumi wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Ndugu Wanawarsha,
Nimeyasema yote haya ili kusisitiza umuhimu wa warsha yenu na kuwataka washiriki wote, na hasa wakufunzi ama wawezeshaji na wakurufunzi, yaani nyie mnaofundishwa, kuyachukulia kwa uzito wa juu kabisa mafunzo haya na programu hii kwa ujumla wake.
Ndugu Wanawarsha,
Baada ya maelezo haya machache, sasa natamka kwamba warsha ya mafunzo ya ukusanyaji wa takwimu za ubunifu wa sanaa na utamaduni kwa nchi ya Tanzania 

IMEFUNGULIWA RASMI.

No comments

Powered by Blogger.